Shirika lisilokuwa la kiserikali la World Vision Tanzania limekabidhi vitanda 100 na magodoro 100 katika shule ya sekondari Simiyu wenye thamani ya shilingi milioni 26.6.
Akikabidhi msaada huo kaimu meneja wa klasta ya Nzega, Bi. Gilselda Balyagati amesema kuwa shirika hilo limeamua kuunga jitihada za serikali ya awamu ya tano za kuhakikisha watoto wanapata elimu bora ngazi ya shule ya Msingi na sekondari ambapo kupitia mradi wa Kanadi limeweza kupata fedha kiasi za kusapoti ununuzi wa vitanda na magodoro kwa wanafunzi wa bweni hasa wasichana ili kuwawezesha kusoma katika mazingira bora.
Aidha, Balyagati amesema kuwa lengo la kutoa msaada huo ni kuchangia na kusaidia juhudi za kuwalinda wasichana dhidi ya vishawishi na mapambano dhidi ya ndoa na mimba za utotoni, huku akibainisha kuwa katika mkoa wa Simiyu shirika hilo lina miradi 5 kwenye afya na maji.
Akizungumza kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka mara baada ya kupokea msaada huo na kuukabidhi kwenye uongozi wa shule ya Sekondari Simiyu, Mkuu wa wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga ameishukuru World Vision kwa msaada huo na kuwataka wanafunzi kutumia msaada huo wa magodoro na vitanda kuongeza ari ya kujisomea na baadaye waweze kufikia malengo yao.
Awali akizungumza kabla ya kumkaribisha Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga Afisa wa Mkoa wa Simiyu, Mwl. Ernest Hinju amesema vitanda hivyo vitasaidia kuboresha mazingira ya kujisomea kwa wanafunzi kwa kuwa shule hiyoimeteuliwa kama kituo cha kambi za kitaaluma.
Hinju ameongeza kuwa kupitia juhudi serikali ya mkoa na wadau watoto wameweza kukaa kambi na hivyo kupata muda wa kutosha kujisomea na kusaidia kupunguza daraja 0 kwenye matokeo ya kidato cha 4 mwaka 2019 na hatimaye kwenye mtihani wa taifa na kufanikiwa kuingia kwenye nafasi ya 5 bora kitaifa.
Kwa upande wake mwl wa shule ya Sekondari Simiyu Vestina Sedekia alilishukuru shirika hilo kwa kutoa msaada huo na kuongeza kuwa wamewasaidia wanafunzi hususan wasiokuwa na uwezo wa kuwa nayo.
"msaada huu ni wa muhimu unakuta familia ina godoro moja la kulalia watoto hata 4 hivyo inakua vigumu mtoto anayetaka kwenda bweni (kambi) kubeba lile godoro na awaache wenzake hawana la kulalia hivyo msaada huo ni wa muhimu "alisema mwl Sedekia
MWISHO
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa