Waziri wa Katiba na Sheria, Balozi Dkt. Augustine Mahiga amevitaka vyombo vya utoaji haki hapa nchini ikiwemo jeshi la polisi na Mahakama kutochelewesha utoaji wa haki ili kuepuka msongamano wa mahabusu katika magereza na badala yake vyombo hivyo vitende haki na kwa wakati.
Waziri Mahiga ameyazungumza hayo leo Julai 14, 2019 wakati akizungumza na waandishi wa habari Mjini Bariadi mara baaada ya kuhitimisha ziara yake na Mkurugenzi Mkuu wa Mashtaka, Biswalo Mganga mkoani Simiyu ambayo ililenga kujionea mazingira ya utoaji haki na haki jinai katika mikoa ya Simiyu na Mara.
“Kuna ucheleweshaji wa kutoa haki kabla mahabusu hajapelewa mahakamani, unaweza kuwa miezi sita, mwaka mmoja na wengine hata miaka miwili bado wanasubiri kwenda mahakamani; hilo nalo linachangia si tu uchache na nafasi ndani ya gereza lakini pia utaratibu wa upelelezi unachelewa ili kukamilisha mashtaka,lakini pia kazi za mahakimu zinatakiwa ziende haraka ili kupunguza mrundikano wa kesi” alisema Waziri Mahiga.
Aidha, Dkt. Mahiga amesema katika ziara hiyo pia wamebaini kuwa katika mikoa ya Simiyu na Mara mahabusu wengi wanakabiliwa na kesi za kuingilia hifadhi ya Taifa ya Serengeti, wizi wa mifugo, ugomvi utokanao na wizi wa mifugo na matatizo yatokanayo na jamii.
Ameongeza kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mashtaka (DPP), Biswalo Mganga kwa mamlaka aliyopewa na sheria ya kusamehe baadhi ya makosa kwa utaratbiu na vigezo Fulani, katika kila Gereza walilopita DPP aliweza kuwasamehe baadhi ya mahabusu kwa kuzingatia vigezo kadhaa ambavyo ni wazee waliozidi miaka 70, watoto chini ya miaka 18, watu wenye ulemavu na wale wenye makosa madogo kama wizi wa kuku na wamekaa mahabusu kwa muda mrefu.
Akitoa taarifa kwa waandishi wa habari, Mkurugenzi Mkuu wa Mashtaka(DPP), Biswalo Mganga amesema pamoja na vigezo vilivyotajwa na waziri Mahiga baadhi ya wahabusu walioachiwa ni wale waliopelekwa gerezani au mahakamani wakati hawakustahili ikiwa ni pamoja na wale waliobambikiwa kesi.
“Kwa hapa Bariadi kuna kesi 46 ambazo zina watu wanaoweza kufika 100, Tarime nako ni watu wengi kidogo lakini idadi haitusaidia, itoshe kusema kuna watu walioachiwa baada ya kuangalia vigezo fulani; kuna watu wanapelekwa mahakamani ambao pengine hawakustahili, ni kwa sababu ya kubambikiwa kesi, mfano mtu amekopa fedha na baada ya kushindwa kulipa badala ya kupelekwa kwenye kesi ya madai, mdai anampeleka polisi kumshtaki kwa kujipatia fedha kwa udanganyifu” alisema DPP.
Kwa upande wake mmoja wa wananchi Mjini Bariadi, Hangi Sapoti amesema ili kuzuia msongamano katika magereza ameshauri mahakama na jeshi la polisi kujiridhisha kabla ya kuwapeleka mahabusu gerezani na ikiwa watuhumiwa wamefanya makosa yanayoruhusu kupewa dhamana wapewe ili wabaki wale tu ambao wamefanya makosa yasiyo na dhamana.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI FUNGUA KIUNGANISHI HIKI:-https://simiyuregion.blogspot.com/2019/07/waziri-mahiga-avitaka-vyombo-vya-utoaji.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa