Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini ametoa wito kwa Taasisi, mashirika ya Umma na binafsi na wadau wote wa kilimo, mifugo na uvuvi wanaotarajia kushiriki maonesho ya Kitaifa ya Nanenane mwaka huu kuanza maandalizi ya maonesho hayo.
Sagini ameyasema hayo jana mara baada ya kukagua na kuona hali ya maandalizi ya maonesho hayo katika Viwanja vya Nyakabindi katika maeneo ya wadau mbalimbali wa maonesho hayo.ambayo yatafanyika kwa mara ya tatu mfululizo katika Kanda ya Ziwa Mashariki Viwanja vya Nyakabindi Bariadi Mkoani Simiyu.
“Halmashauri za mikoa ya Simiyu, Mara na Shinyanga ambayo ndiyo inaunda Kanda ya Ziwa Mashariki zimeanza vizuri, taasisi zilizo chini ya Wizara ya kilimo nazo zimefanya vizuri lakini baadhi ya wadau wa sekta ya kilimo hawajajitokeza; nitoe wito kwa wadau wote watakaoshiriki katika maonesho ya Nanenane Kitaifa mwaka huu mkoani Simiyu waweze kuja kuanza maandalizi,” alisema Sagini.
Amesema maandalizi ya vipando vya mazao, mashamba darasa, mabanda ya mifugo na mabwawa ya samaki yanahitaji muda hivyo ni vema wakaanza mapema ili kupata vitu vizuri vitakavyotumika kuelimisha wakulima, wafugaji na wavuvi kuhusu teknolojia rahisi zinazotumika katika uzalishaji wenye tija.
Mkurugenzi wa maendeleo ya mazao kutoka wizara ya kilimo, Bw. Nyasebwa Chimagu amesema ameridhishwa na maandalizi ya maonesho ya nane nane huku akiwataka wadau kuyatumia kama kichecheo kikubwa cha ueneaji wa technolojia za kisasa katika sekta ya kilimo, mifugo na uvivu ili mazao yao yaweze kuwa na tija.
Pamoja na kukiri kuwa hamasa ya maandalizi ya maonesho ya Nanenane mwaka 2020 ilishuka baada ya kuibuka kwa homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi vya corona, Chimagu amesema kuwa kwa sasa maandalizi yanaendelea katika viwanja vyote nane vya kanda za maonesho hayo nchi nzima.
Aidha Chimagu amewatoa hofu wananchi wote juu ya sintofahamu ya maonesho ya nane nane na kusema kuwa yatakuwepo na kuwasisitiza wadau ambao hawajajitokeza kujitokeza kwenye viwanja vya maonesho kwa ajili ya kuanza shughuli za maandalizi kwani tayari wengine wameanza na maendeleo ni mazuri.
"Niwatoe hofu wananchi wote nchini kuwa maonesho ya nanenane yatakuwepo kwenye viwanja vyote vya kanda, kitaifa yatafanyika mkoani Simiyu kwa mara ya tatu mfululizo, hivyo wadau binafsi, taasisi za umma na binafsi pamoja na halmashauri ambazo bado hazijaanza maandalizi kuanza shughuli za maandalizi ya maonesho, "alisema Chimagu.
Kwa upande wake Bwana shamba kutoka Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Ishengoma Julius amesema maandalizi ya vipando kwa ajili ya maonesho ya nane nane yamefikia 75% na vipando vya muda mfupi vimebaki kwa 25% na kusema kuwa mpaka kufikia maonesho hayo vitakuwa tayari.
Naye mkuu wa kambi ya jeshi la magereza kwenye maonesho ya nane nane Nyakabindi, Bw. Patrick Matiku amesema wanafanya ukaguzi kila siku kwenye vipando vyao ili waweza kubaini kama kuna tatizo na kulitatua mapema.
Maonesho ya Nanenane mwaka 2020 yanaongozwa na Kauli Mbiu inayosema “KWA MAENDELEO YA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI CHAGUA VIONGOZI BORA 2020”.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI FUNGUA KIUNGANISHI HIKI:-https://simiyuregion.blogspot.com/2020/05/washiriki-nanenane-kitaifa-mwaka-2020.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa