Jumla ya wakazi 2228 wa mji wa Lagangabilili Wilayani Itilima wanatarajia kuondokana na adha ya kupata huduma ya maji umbali mrefu baada ya kukamilika kwa ujenzi wa chanzo cha maji ya bomba chenye uwezo wa kutoa maji kiasi cha lita za ujazo 15000 kwa saa.
Chanzo hicho cha maji chenye mtandao wa mabomba ya maji ya urefu wa mita 29,431 na vituo vya kuchotea 20 vitawasaidia wananchi hao kupunguza muda waliokuwa wakiupoteza kufuata huduma ya maji umbali wa kilometa zaidi ya mbili
Akisoma taarifa ya ujenzi wa mradi huo wa maji kwa kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Ndg.Amour Hamad Amour,mhandisi wa maji wa Halmashauri ya Itilima Goodluck Masige amesema kuwa wananchi wa mji wa lagangabilili wamekuwa wakifuata maji kwa umbali mrefu hali inayopelekea kupoteza muda mwingi ambao wangetumia kutekeleza shughuli za maendeleo.
Masige amesema kuwa mradi huo ambao utagharimu jumla ya shilingi milioni 978 hadi kukamilika kwake utasaidia kupunguza tatizo la uhaba wa maji kwa wananchi, ambapo amesema pamoja na kuwaduhumia wananchi utaweza kutoa huduma ya maji kwa taasisi mbalimbali katika Mji wa Lagangabilili na kunywesha mifugo.
Aidha kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru Amour Hamad Amour amesema amefurahishwa sana na mradi huo ambao utawatua ndoo vichwani akinamama na kuwapumzisha mzigo mzito waliokuwa wakiubeba kwa kipindi kirefu.
"Nimefurahishwa sana na mradi huu...ni mradi ambao utakuwa na manufaa makubwa katika ustawi wa maendeleo ya wananchi sambamba na kuwatua akinamama hawa ndoo kichwani,jambo ambalo ni azma ya Serikali ya awamu ya Tano “ amesema
Aidha, kiongozi huyo amemtaka Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Itilima kuunda kamati za watumia maji ili kuboresha huduma za utoaji maji kwa wananchi wote bila kujali tofauti za kiitikadi, dini ,rangi siasa wala kabila na kusimamia utunzaji wa miradi yote ya maji.
Sambamba na hilo Ndg.Amour Hamad Amour akiweka jiwe la Msingi katika jengo la Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Itilima amepongeza Wakala wa Majengo wa Taifa(TBA) kwa kujenga jengo kubwa lenye vyumba zaidi ya 40 katika ubora wa hali ya juu kwa gharama nafuu.
Ndg.Amour amesema jengo hilo litakapokamilika watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Itilima walitumie vizuri kwa kutoa huduma bora kwa wananchi kwa uadilifu na kuacha mazoea katika utendaji.
Pamoja na kuweka jiwe la Msingi katika Chanzo cha Mradi wa Maji Lagangabilili na Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya, Mwenge wa Uhuru ukiwa Wilayani Itilima umezindua vyumba vinne vya madarasa na klabu ya wapinga rushwa shule ya sekondari Budalabujiga,kuweka jiwe msingi Bweni la Wavulana Kanadi Sekondari na kuona maboresho ya viwanda na utunzaji wa mazingira kwa ufugaji wa nyuki.
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa