Walimu wa Shule za Msingi Mkoani Simiyu wameiomba Serikali kushughulikia changamoto ya ukosefu wa vitabu vya darasa la nne ili waweze kutimiza wajibu wao vema wa kuwafundisha wanafunzi jambo ambalo Serikali ya Mkoa imelipatia majibu.
Ombi hilo limetolewa kwa Serikali wakati wa kikao kati ya Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka na walimu wa Shule ya msingi Somanda A na Somanda B ambacho kimefanyika katika Shule ya Msingi Somanda A Mjini Bariadi.
Wakiongea katika kikao hicho wamesema kutokana na kutokuwepo kwa vitabu vya mtaala ulioboreshwa wamekuwa wakitumia vitabu vya mtaala wa zamani katika kuwafundisha wanafunzi, hivyo wanaomba serikali iwaletee vitabu vipya ili waweze kuendana na mahitaji ya mtaala uliboreshwa.
“Wakati mwingine tunalazimika kuwafundisha watoto kwa kutumia vitabu vya mtaala wa zamani, badala ya kuwapa watoto kile wanachostahili tunawapa kilichopitwa na wakati, tunaomba tupate vitabu vya vipya ili kuendana na mtaala uliopo katika kuwapa watoto kile wanachostahili” alisisitiza Mwl.Francis Paulo kutoka Shule ya Msingi Somanda A.
Kwa upande wao wadhiti Wakuu wa Ubora wa Shule, Hellen Jackson kutoka Halmashauri ya Mji wa Bariadi na Fabian Machunde kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Bariadi wamekiri kuwepo kwa tatizo la upungufu wa vitabu vya darasa la nne jambo ambalo lina athari kwa wanafunzi hususani katika ujifunzaji .
“Ni kweli kukosekana kwa vitabu shuleni kuna athari kubwa kitaaluma mwalimu anahitaji vitabu na mwanafunzi pia anahitaji vitabu anapofundishwa darasani na kujisomea ili kuongeza maarifa zaidi ya yale aliyojifunza darasani” alisema Hellen Jackson.
Naye Mkoa wa Simiyu, Mhe.Anthony Mtaka baada ya kuwasikiliza walimu pamoja na wadhibiti Ubora Mkuu hao, amesema Taasisi ya Elimu Ukuzaji Mitaala inapaswa kutimiza wajibu wake katika kuhakikisha inaleta vitabu hivyo katika Mkoa huo, ili walimu na wanafunzi wapate vitabu na kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia.
“Kama Taasisi ya Ukuzaji Mitaala Tanzania imeshindwa kuleta vitabu vya darasa la nne kwa miezi tisa sasa hawana uhalali wa kuwepo, huyo Mkurugenzi wa Taasisi anaingia Ofisini kufanya kazi gani kama anajua nchi nzima haina vitabu vya darasa la nne, atafutwe mtu mwingine atakayekuja na maarifa mapya akubali maoni ya mikoani” alisema Mtaka.
Ameongeza kuwa ili walimu waweze kupimwa utendaji wao wa kazi ni lazima wawe na vitabu vya kufundishia na ili wanafunzi waweze kupimwa kiwango chao cha ufaulu ni lazima wawe na vitabu vya kujifunzia, hivyo ikiwa Taasisi hiyo haina uwezo wa kuchapicha vitabu hivyo kwa sasa iupelekee mkoa wa Simiyu nakala zilizohaririwa na mkoa utaweka utaratibu wa kuchapisha vitabu hivyo.
Aidha, Mtaka amesema walimu, viongozi pamoja na wadau mbalimbali wa elimu mkoani Simiyu wamefanya jitihada kubwa katika kuboresha elimu jambo ambalo limeutoa mkoa huo kufanya vibaya katika mitihani ya Kitaifa ukiwepo wa darasa la nne, hivyo ni vema jitihada hizo zisirudhishwe nyuma kwa namna yoyote.
Afisa Elimu Mkoa wa Simiyu amesema pamoja na kuwepo kwa ukosefu wa vitabu vya darasa la nne Serikali imetoa vitabu kwa madarasa mengine ikiwemo vitabu vya najifunza kusoma (darasa la kwanza) lakini mgawanyo wa vitabu hivyo haukuwa mzuri, akaomba ufanyike utaratibu kila mkoa upate nakala chache.
Mkoa wa Simiyu kwa sasa unahitaji vitabu zaidi ya 50,000 kwa ajili ya kufundishia na kujifunzia kwa wanafunzi wa darasa la nne.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI JUU YA HABARI HII FUNGUA HAPA:-https://simiyuregion.blogspot.com/2018/02/walimu-simiyu-waililia-serikali-ukosefu.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa