Takribani vijana 664 mkoani Simiyu wanatarajia kunufaika na ajira za muda katika msimu huu ,baada ya kupata mafunzo ya matumizi sahihi ya viuatilifu kwa ajili ya kukabiliana na wadudu wasumbufu wa zao la Pamba.
Hayo yamebainishwa jana Novemba 24, 2020 wakati wa kufunga mafunzo ya matumizi sahihi ya viuatilifu kwa wapuliziaji sumu katika zao la pamba yaliyotolewa na Gatsby Africa kwa kushirikiana na Taasisi ya Utafiti na Udhibiti wa Viuatilifu (TPRI) katika Halmashauri zote sita za Mkoa wa Simiyu ambayo yalihitimishwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bibi. Miriam Mmbaga.
Vijana hao wamebainisha mafunzo waliyoyapata pamoja na kuwasaidia kupata ajira yatawawezesha kuongeza tija katika uzalishaji wa pamba kwa kuwa wamefahamu matumizi sahihi ya viuatilifu ilinganishwa na awali walipokuwa wakifanya kazi hiyo kienyeji.
“Tulikuwa tunafanya kienyeji lakini kwa sasa tumepata ujuzi mfano tumejifunza ni dawa ipi inatumika kuua aina gani ya wadudu kwa wakati gani; lakini pia tumejifunza ni kwa namna gani tunaweza kutumia viuatilifu pasipo kuathiri mazingira yetu,” alisema Samwel Salum mpuliziaji viuatilifu vya zao la pamba Meatu.
“Mafunzo haya kwangu yana umuhimu mkubwa sana maana nitakuwa nikipulizia viuatilifu kwenye mashamba ya wakulima napata hela, lakini pia nitatumia mbinu nilizojifunza kupulizia kwenye mashamba yangu na nitaongeza uzalishaji,” alisema Mayunga Mlyaza mpuliziaji viuatilifu vya zao la pamba Meatu.
Afisa Kilimo wa Kata ya Sakasaka Wilayani Meatu, Sylvester Mholi amesema mafunzo hayo yamewaongezea uwezo wa kujiamini katika kutambua viuatilifu ambavyo vinasambazwa na wasambazaji kwa kuzingatia sheria na miongozo mbalimbali inayohitajika.
Mwakilishi wa Gatsby Africa shirika lililoshirikiana na Mkoa kuandaa mkakati wa mapinduzi kilimo cha pamba (2019-2024) katika mafunzo hayo Bw.Michael Kahindi amesema wakulima waliofikiwa na wapuliziaji hawa wa viuatilifu katika msimu uliopita wamefanikiwa kuongeza tija katika Uzalishaji wa pamba kutoka kilo 250 mpaka kufikia kilo 600 kwa hekali.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bibi. Miriam Mmbaga amesisitiza uadilifu wakati wa utekelezaji zoezi la upuliziaji dawa katika mashamba ya wakulima “tusifanye udanganyifu kwa wakulima, ukimdanganya mteja wako kesho hatarudi tena kwako; sisi kama mkoa tunaona fahari kuwa tunao vijana 664 ambao tumewaongezea thamani kwenye kazi walizonazo.”
Mtafiti wa kudhibiti visumbufu vya mazao/mimea kutoka Taasisi ya Utafiti wa viuatilifu nchini(TPRI), Bw. Ramadhan Kilewa amesema matarajio ya TPRI ni kuwa vijana hao wataenda kufanya kazi nzuri baada ya mafunzo hayo kwa kuwa awali baadhi yao walieleza kuwa walikuwa wakifanya kazi hiyo tofauti na maelekezo ya matumizi sahihi ya viuatilifu.
Kwa upande wake kaimu Katibu Tawala Msaidizi-Seksheni ya Uchumi na Uzalishaji, Bibi. Kija Kayenze amesema “Lengo ni kuongeza tija hivyo tunatarajia tija itaongezeka sana kwa sababu wakulima wengi watakuwa wameshapata elimu sahihi ya matumizi ya viuatilifu.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI FUNGUA KIUNGANISHI HIKI:-
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa