Changamoto ya upungufu wa damu kwa wanawake wenye umri wa kuzaa mkoani Simiyu imepungua kutoka asilimia 57 mwaka 2015 hadi kufikia asilimia 34 mwaka 2019 kutokana na juhudi mbalimbali zilizofanywa na viongozi, watendaji na wananchi, ikiwa ni pamoja na kulipa kipaumbele suala la lishe.
Hayo yamebainishwa na Afisa Lishe wa Mkoa wa Simiyu, Dkt. Chacha Magige wakati akiwasilisha taarifa katika kikao cha kamati ya lishe ya mkoa kilichofanyika jana Novemba 11, 2020 mjini Bariadi.
Magige amesema Elimu ya kujirudiarudia imewafanya wananchi wapate uelewa wa kutosha juu ya ulaji sahihi ambapo amesisitiza kuwa pamoja na elimu mkoa uliweka mkakati kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kuongeza nguvu katika katika utoaji wa vidonge vya kuongeza damu kwa wasichana.
“Suala la lishe limepewa kipaumbele katika mkoa wetu na elimu inaendelea kutolewa katika vituo vya kutolea huduma za afya, ngazi ya jamii ambapo wanawake wanafundishwa kuandaa chakula kwa usahihi katika makundi yote matano ya vyakula,” alisema Dkt. Magige.
Katika hatua nyingine Magige amesema katika kukabiliana na udumavu mkoani Simiyu, Mkoa umejiwekea mikakati kadhaa ikiwa ni pamoja na kutoa elimu ya namna ya kuandaa vyakula vya kuwalisha watoto walio vituo vya kutolea huduma za afya na ngazi ya jamii, elimu ya unyonyeshaji sahih, elimu ya mabadiliko ya ulaji na kuhimiza wananchi kwenda kuapata matibabu katika vituo vya kutolea huduma za afya.
Akizungumza na wajumbe wa kamati ya lishe ya mkoa, Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu Bibi. Miriam Mmbaga ametoa rai kwa viongozi na watendaji kuendelea kutimiza wajibu wao na kila mmoja kutambua kuwa suala la lishe ni la muhimu huku akisisitiza ushirikiano ili kuwaokoa wananchi wa mkoa wa Simiyu kuondokana na athari zitokanazo na lishe duni.
Kwa upande wake Afisa Lishe wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega, Bi. Happiness Kubona amesema Maafisa Lishe wataendelea kuwajengea uwezo wahudumu wa afyangazi ya jamii, ngazi ya vituo kuwatambua watoto wenye utapiamlo na kuwaingiza katika matibabu .
Ameongeza kuwa hamasa ya kujiunga na Mfuko Afya ya Jamii ulioboreshwa(ICHF) kwa wananchi itaendelea kutolewa ili waweze kupata huduma za matibabu na hususani wanawake waweze kupata huduam ya vidonge vya kuongeza damu ili wasipungukiwa damu wakati wa ujauzito.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI FUNGUA KIUNGANISHI HIKI:-https://simiyuregion.blogspot.com/2020/11/upungufu-wa-damu-kwa-wanawake-wenye.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa