Mkoa wa Simiyu umeanzisha mfumo rasmi wa ukusanyaji takwimu na utunzaji wa kumbukumbu za wakulima wa pamba uitwao ‘Kilimo Maendeleo’ utakaowawezesha wakulima kusajiliwa katika Vyama vya msingi vya Ushirika (AMCOS), kuuza pamba yao kwa njia ya mtandao na kupata pembejeo zote kutoka kwa wauzaji wa pembejeo.
Akizungumza katika uzinduzi wa mafunzo juu ya mfumo huo, Meneja wa huduma za ugani kutoka GATSBY AFRICA, Bw. Sunday Mtaki amesema Mfumo huo utaanza kutekelezwa katika AMCOS 24 zilizoteuliwa kwa kuanzia.
“Katika utekelezaji wa mkakati wa miaka mitano ya mkoa wa Simiyu katika zao la pamba, eneo la usajili wa wakulima na matumizi ya TEHAMA kwenye kilimo ni muhimu sana, tumeileta kampuni inaitwa LITENGA ambayo ina mtandao unaitwa Kilimo Maendeleo kazi yake ni kuwaunganisha wakulima kupitia AMCOS na taarifa zote za mkulima zitapatikana kupitia simu za mkononi,” alisema Mtaki.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu amesema mfumo huo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango mkakati wa miaka mitano wa kilimo cha zao la pamba ulioandaliwa na Mkoa kwa kushirikiana na wadau, kwa lengo la kuboresha kilimo cha pamba, huku akiwataka Maafisa Kilimo na Maafisa ushirika kutimiza wajibu wao.
“Maafisa Kilimo na Maafisa Ushirika timizeni wajibu wenu msisubiri mgombane na mtu hii kazi ndiyo inayowapa heshima, Serikali ya Rais Magufuli imeweka mkakati wa kuhakikisha zao la pamba linakuwa zao muhimili kwenye nchi yetu, ndiyo maana sisi kama Mkoa tumeanza utekelezaji wa mkakati wa miaka mitano wa kilimo cha zao la pamba,” alisema Mtaka.
Aidha, Mtaka ameongeza kuwa dhamira ya mkoa ni kufanya mapinduzi katika kilimo cha pamba ili wakulima walime kilimo cha kisasa chenye tija na kuwa na ushirika imara, ambapo amesema viongozi wa AMCOS wasio waaminifu watachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria ikiwa ni pamoja na kuwavua nyadhifa zao.
Mwenyekiti wa Chama cha Ushirika cha Mkoa wa Simiyu (SIMCU), Bw. Charles Madata amewaonya viongozi wa AMCOS kuwa waaminifu na kuhakikisha kila mmoja anakuwa na nidhamu ya fedha ili mali za wakulima ziweze kuwa salama.
Kwa upande wake Kaimu Mrajisi wa Vyama vya Ushirika Mkoa wa Simiyu, Bw. Ibrahimu Kadudu amesema viongozi wote wasio waaminifu watachukuliwa hatua, ambapo amebainisha kuwa takribani viongozi 107 wa AMCOS wilayani Maswa waliohusika na ubadhilifu wanatarajiwa kufikishwa mahakamani mara baada ya kukamilika kwa ukaguzi.
Naye Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini amesema kupitia mkakati wa miaka mitano ya mkoa wa Simiyu katika zao la pamba, mkoa wa huo unatarajia kuongeza tija ya uzalishaji wa pamba kutoka kilo 200 kwa ekari hadi kufikia kilo 600 hadi 1000 au zaidi kwa ekari.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI FUNGUA KIUNGANISHI HIKI:-https://simiyuregion.blogspot.com/2019/10/simiyu-kuanzisha-mfumo-wa-ukusanyaji.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa