Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amezindua zoezi la utoaji wa chanjo ya Surua-Rubella kwa watoto wenye umri kuanzia miezi tisa hadi miezi 59 (chini ya miaka mitano) na kuwahimiza wananchi kuwapeleka watoto kupata chanjo hiyo inayotolewa bila malipo kwenye vituo vya kutolea huduma za afya na vituo vya muda vilivyotengwa vipatavyo 405, ili kuwakinga watoto hao na maradhi.
Akizungumza na wananchi walioshiriki katika uzinduzi wa zoezi hilo Oktoba 17, 2017 katika Kituo cha Afya cha Muungano Mjini Bariadi, Mtaka amesema ni vema wananchi hao watumie siku zilizotengwa kutoa chanjo hiyo kuanzia Oktoba 17-21, 2019 kuwapeleka watoto kwenye chanjo na wawe mabalozi wema kwa wenzao.
“Madhara ya Surua ni pamoja na masikio ya mtoto kutoa usaha utakaosababisha mtoto kuwa kiziwi, vidonda vya macho vinavyoweza kusababisha upofu, utapiamlo, kuvimba ubongo, udumavu wa akili na kifo; mliokuja leo mkawe mabalozi wema kwa wenzenu wawalete watoto chanjo ili watoto wakingwe dhidi ya haya magonjwa,” alisema Mtaka.
Katika hatua nyingine Mtaka amewataka wananchi kutumia vituo vya kutolea huduma za afya vilivyopo kwenye maeneo yao kupata huduma za matibabu ili waweze kupata tiba sahihi kwa wakati sahihi badala ya kwenda kwa waganga kupiga ramli.
Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Dkt. Festo Dugange amesema watoto takribani 420,000 wanatarajiwa kupata chanjo ya Surua-Rubella, ambapo chanjo hiyo itakuwa ikitolea kuanzia saa moja asubuhi hadi saa 12 jioni.
Kwa upande wake mmoja wa wazazi waliowapeleka watoto wao kwenye Bw. Hamza Adam amesema ni vema kila mzazi mwenye mtoto wa umri chini ya miaka mitano ampeleke akapate chanjo ya Surua-Rubella, ili wawakinge na maradhi hayo na kuwaomba wasiwapeleke kwa waganga wa jadi wanapokuwa wagonjwa.
Mwenyekiti wa Mtaa wa Benki Mjini Bariadi, Consolata Cosmas amesema wenyeviti wa Mitaa na Vijiji mkoani Simiyu wameshiriki kikamilifu katika kuhamasisha waananchi kupeleka watoto kupata chanjo, hivyo imani yao ni kwamba zoezi hilo litafanikiwa kwa kuhakikisha watoto wote waliopangwa kupewa chanjo wanapewa na lengo linafikiwa.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI FUNGUA KIUNGANISHI HIKI:-https://simiyuregion.blogspot.com/2019/10/rc-mtaka-awahimiza-wananchi-simiyu.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa