Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amewahakikishia waumini na viongozi wa madhehebu ya dini mkoani hapa kuwa viongozi wa serikali wako pamoja nao na wataendelea kushirikiana na kila watakapo wahitaji .
Mtaka ameyasema hayo jana Mei 30, 2019 katika futari aliyoiandaa kwa waumini na viongozi wa madhehebu ya Kiislam katika Viwanja vya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Mjini Bariadi.
“Ndugu zangu waislam mliopo hapa naomba muamini kabisa kwamba viongozi wa mkoa na viongozi wote wa Serikali kwenye maeneo yetu ndani ya mkoa wa Simiyu wako pamoja na ninyi; kwa jambo lolote, eneo lolote ambalo mngehitaji ushirikiano kwenye mkoa wetu sisi tuko tayari kuunga mkono” alisema Mtaka.
Aidha, ameshauri viongozi wa BAKWATA Mkoa wa Simiyu kuomba kuandaa tukio moja kubwa la Kitaifa kufanyika Mkoani Simiyu kama ambavyo yamekuwa yakifanyika katika mikoa mingine na akaahidi kushirikiana na viongozi hao endapo watakuwa tayari kuandaa tukio lolote.
Katika hatua nyingine Mtaka ametoa wito pia kwa viongozi wa Madhehebu ya Kiislam kutengeneza mazingira mazuri kwa vijana na kuwafundisha ikiwa ni njia moja wapo ya kuwaandaa kushiriki katika mashindano ya kuhifadhi Quran ili Mkoa wa Simiyu na nchi kwa ujumla iweze kuwakilishwa vema katika mashindano hayo.
Sambamba na hilo amewashukuru viongozi wa dini kwa kuendelea kuiombea nchi, viongozi wake, kuombea amani, umoja na mshikamano miongoni mwa Watanzania ambapo amebainisha kuwa Serikali inatambua mchango wa Taasisi za dini katika nchi na kwa namna viongozi wa dini wanavyoshirikiana na Serikali katika masuala na mtukio mbalimbali.
Kwa upande wake Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mahamoud Kalokola amemshukuru Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka kwa namna anavyoenzi waislam na akatoa wito kwa watu wengine kuiga mfano wake kwa kuwa kila anyefanya hivyo anapata thawabu yake kwa Mwenyezi Mungu.
Ameongeza kuwa tendo hilo la kufuturisha linawakusanya watu pamoja walio waislam na wasio waislam jambo ambalo linadumisha umoja, upendo, ushirikiano na mshikamano kwa wote bila kujali tofauti ya dini zao.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Mhe. Festo Kiswaga amempongeza Mkuu wa mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka ambao nao watajipanga kufanya jambo hili ili nao waweze kupata baraka za Mwenyezi Mungu.
Huu umekuwa ni utaratibu kwa Mkuu wa mkoa wa Simiyu, kuandaa furati kwa waumini viongozi wa madhehebu ya dini ya Kiisla, ambayo pia huwahusisha viongozi wengine wa chama na Serikali wakati wa mfungo wa mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI FUNGUA KIUNGANISHI HIKI:-https://simiyuregion.blogspot.com/2019/05/mkuuwa-mkoa-wa-simiyu-mhe.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa