Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amesema atatoa kiasi cha shilingi bilioni nne kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa hospitali ya Mkoa wa Simiyu na kuutaka Wakala wa Majengo hapa nchini (TBA) kujenga majengo hayo usiku na mchana, ili kuhakikisha yanakamilika katika kipindi cha meizi sita kama ilivyoahidiwa na Waziri wa Afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto, Mhe. Ummy Mwalimu.
Mhe. Rais Magufuli ameyasema hayo Septemba 08, 2018 katika Uzinduzi wa Jengo la Wagonjwa wa Nje la Hospiali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu katika mtaa wa Nyaumata mjini Bariadi, wakati akiwa katika ziara yake ya siku tatu mkoani humo.
Dkt Magufuli amesema kuwa atatoa shilingi bilioni nne ambazo zitasaidia kujenga majengo mengine ili wananchi wa Mkoa wa Simiyu na maeneo jirani waweze kupata huduma za rufaa huku akieleza kuwa kutokana na umuhimu wa sekta ya afya shirika la Global fund wametoa shilingi bilioni 1.5.
“Leo ninafungua jengo hili na nakugiza Mhe. Waziri wasaidizi wako na TBA anzeni kupima majengo mengine yote yaliyobaki muanze leo fedha zitatatolewa, zipo za global fund bilioni1.5 zipo za Serikali bilioni 1.5 na mimi nawaongezea nyingine bilioni nne ziwe bilioni saba, ninachowaomba TBA mjenge usiku na mchana” alisema.
Awali akitoa taarifa ya Ujenzi wa Jengo la Wagonjwa wa Nje la Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu mjini Bariadi Waziri wa Afya,jinsia ,wazee na watoto Mhe. Ummy Mwalimu amesema kuwa jengo hilo lianza kujengwa Novemba 2015 na kukamilika Mei 2018, limegharimu kiasi cha bilioni 2.1 ikiwemo na fidia ya eneo.
Ameongeza kuwa Wizra ya Afya itahakikisha miundombinu yote muhimu ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa inakamilika, ili Hospitali hiyo iweze kutoa huduma bora kwa wananchi, ambapo amebainisha kuwa hospitali hiyo itapunguza mlundikano wa wagonjwa katika Hospitali Teule ya Mkoa ambayo ina hadhi ya Hospitali ya Wilaya.
Aidha, Mhe. Waziri Ummy amemuahidi Mhe. Rais kuwa yeye kwa kushirikiana na wasaidizi wake watahakikisha majengo ambayo yatajengwa kwa kutumia fedha aliyoahidi kuitoa yanakamilika ndani ya kipindi cha miezi sita, ambapo alisema kwa sasa huduma za wagonjwa wa nje, huduma za dharura, usatwi wa jamii na huduma za maabara vipimo vya kawaida zinatolewa
Ummy pia alibainisha kuwa katika bajeti ya mwaka 2018/2019, Serikali imetenga kiasi cha shilingi Bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Mkoa ambayo kukamilika kwake kutawapunguzia wananchi wa Simiyu kufuata huduma za rufaa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando jijini Mwanza.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amesema katika mwaka wa fedha 2017.2018 mkoa wa Simiyu umepokea shilingi bilioni 11 kwenye sekta ya Afya ambapo Vituo vya Afya 39 vimejengwa na kukarabatiwa pamoja na bilioni mbili kwa ajili ya ununuzi wa dawa.
Pamoja na kufungua Jengo la Wagonjwa wa nje (OPD) la Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu, Mhe. Rais Magufuli amefungua Mtandao wa barabara za lami Mjini Bariadi zilizojengwa chini ya mradi wa ULGSP, kuweka jiwe la msingi mradi wa maji Lamadi na kuweka jiwe la Msingi Ujenzi wa Barabara ya Bariadi-Maswa inayojengwa kwa kiwango cha lami yenye urefu wa KM 49.7.
Sepemba 09, 2018 Mhe. Rais Magufuli anaendelea na ziara mkoani Simiyu ambapo atapita na kufanya mkutano wa hadhara Lagangabilili Itilima na kuelekea Meatu.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI KUHUSU HABARI HII FUNGUA KIUNGANISHI HIKI:https://simiyuregion.blogspot.com/2018/09/rais-magufuli-aahidi-bilioni-nne.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa