Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. John Pombe amewaagiza Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi. Isack Kamwelwe na Mtendaji Mkuu wa TANROADS kusimamia Ujenzi wa Daraja la Mto Sibiti linalounganisha mikoa ya Simiyu na Singida na kuhakikisha linakamilika ifikapo Machi, 2019.
Rais Magufuli ameyasema hayo Septemba 10, wakati akizungumza na wananchi wa mikoa ya Simiyu na Singida katika Kijiji cha Nyahaa wilayani Mkalama Mkoani Singida muda mfupi kabla ya kuweka jiwe la msingi ujenzi wa daraja hilo.
Amesema daraja hilo limeanza kujengwa muda mrefu na akazikataa sababu zilizotolewa na Mkandarasi kuwa zimepelekea kuchelewesha ukamilishaji ikiwemo mkandarasi kufanya kazi miezi minne tu kwa mwaka kutokana na eneo hilo kuwa na maji mengi hususani kipindi cha mvua.
"Wananchi wa hapa wanahitaji daraja limalizike hawahitaji sababu, mkandarasi alipokuwa akiomba kazi hakujua kuwa hapa maji huwa yanapita, ma-engineer hawakujua? Hapa hakuna sababu,msitafute kisingizio"
"Mhe. Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote, Mtendaji Mkuu TANROADS nataka daraja hili sasa likamilike, mimekuja kwa makusudi kuweka jiwe la msingi nataka siku nikirudi nipite juu" alisema Rais Magufuli
Kwa upande wake Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi. Isack Kamwelwe amesema Daraja la Mto Sibiti likikamilika litakuwa mkombozi katika kuunganisha mikoa ya Kanda ya Ziwa na mkoa wa Singida na kuahidi ujenzi wa kilomita 25 za lami kwenye tuta la daraja hilo.
"Daraja hili limejengwa katika viwango vya juu sana, tuta lake pia limejengwa kwa kiwango cha juu sana na tayari tumeshaongea na TANROADS kwamba kupitia kwenye fedha za matengenezo, tuta hili kwa karibu kilomita 25 tutaziweka lami Mhe. Rais, tutaposhindwa tutakupa taarifa"
Naye Mtendaji Mkuu wa TANROADS Mhandisi. Patrick Mfugale amesema kazi ya Ujenzi wa Daraja la Mto Sibiti inayofanywa na Mkandarasi Hainan International Limited kutoka nchini China na mpaka sasa umefikia asilimia 70 na hadi kukamilika kwake litagharimu jumla ya shilingi bilioni 16.3.
Rais amehitimisha Ziara yake ya siku tatu mkoani Simiyu Septemba 10, ambapo akiwa Simiyu alipata nafasi ya kuweka mawe ya msingi, kufungua miradi mbalimbali ya maendeleo na kuzungumza na wananchi katika maeneo mbalimbali kupitia mikutano ya hadhara.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI KUHUSU HABARI HII FUNGUA KIUNGANISHI HIKI:https://simiyuregion.blogspot.com/2018/09/rais-magufuli-aagiza-wizara-ya-ujenzi_11.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa