Naibu Waziri wa Kilimo, Mhe. Omary Mgumba ametoa wito kwa wakulima Mkoani Simiyu kuondokana na dhana potofu kuwa matumizi ya mbolea yanazeesha ardhi badala yake wazingatie matumizi sahihi ya mbolea katika kilimo ili kuongeza mavuno, tija na uzalishaji katika kilimo.
Mhe. Mgumba ameyasema hayo Machi 06, 2019 wakati akizungumza na wananchi wilayani Itilima Mkoani Simiyu, katika Mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Bukingwaminzi kata ya Zagayu wilayani humo wakati wa ziara yake ya kikazi mkoani Simiyu.
Ameongeza kuwa siyo kweli kwamba matumizi ya mbolea yanazeesha ardhi badala yake mbolea inasaidia kutibu ardhi na kupelekea wakulima kuongeza mavuno na tija katika uzalishaji wa mazao na kuwawezesha kushindana katika masoko ya ndani na nje ya nchi.
“Nimeambiwa hamtaki kutumia mbolea kwa madai kwamba mkitumia mbolea inazeesha ardhi siyo kweli, mbolea hizi haziharibu ardhi yetu bali zinakwenda kutibu ardhi;ndiyo maana watu wa Ruvuma, Njombe, Iringa, Mbeya , Songwe, Rukwa na Katavi wanaongoza kwa kuzalisha mahindi nchini wenzetu ni wajanja wanatumia Mbolea”alisema
Akizungumzia suala la viuatilifu Mgumba amewahakikishia wakulima wa zao la pamba mkoani Simiyu kuwa tayari bodi ya pamba imeshatoa chupa 1000 za viuatilifu/viuadudu ambapo kila wilaya itapata chupa 200.
Katika hatua nyingine Mhe. Naibu Waziri amezungumzia suala la bei ya pamba ambapo amesema Serikali inaendelea kuandaa mazingira wezeshi kwa wanunuzi wa pamba wa ndani na nje ya nchi kununua pamba ya wakulima kwa bei nzuri na kubainisha kuwa utaratibu utakaotumika ni wa soko huria.
Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Itilima, Mhe. Njalu Silanga pamoja na kuomba pamba iuzwe kwa bei ya soko huria na kuongezewa viuatilifu, ameomba maghala ya kuhifadhia pamba yajengwe kupitia sehemu ya fedha inayotolewa na wakulima katika Vyama vyao vya Ushirika ili pamba ihifadhiwe vizuri na tija ionekane.
Naye Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Mhe. Benson Kilangi amesema jitihada zinaendelea kufanyika kuwahamasha wakulima wote wa pamba kujiunga na vyama vya ushirika ambapo amesema hadi sasa ni wakulima 11,700 kati ya 38,910 wako katika vyama vya ushirika vipavyo 56.
Nao baadhi ya wananchi waliopata nafasi ya kuwasilisha maombi na kero zao kwa Naibu Waziri wa Kilimo wameomba viuatilifu/viuadudu vilivyotolewa na bodi ya pamba viwafikie wakulima kwa wakati.
Naibu Waziri Mgumba yuko mkoani Simiyu katika ziara ya kikazi yenye lengo la kukagua shughuli za kilimo na ushirika zinavyoendelea na kukagua shughuli za miradi ya umwagiliaji akiwa Wilayani Itilima amepata nafasi ya kuzugumza na wananchi kupitia mkutano wa hadhara.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI OFUNGUA KIUNGANISHI HIKI:-https://simiyuregion.blogspot.com/2019/03/naibu-waziri-kilimo-awaasa-wakulima.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa