Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Samia Suluhu Hassan amekemea tabia ya baadhi ya viongozi kuwapa ndugu au jamaa zao zabuni za ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwepo miradi ya maji kwa kuwa ni kinyume cha taratibu na hali hiyo haiwatendei haki wananchi na Serikali.
Mhe.Makamu wa Rais aliyasema hayo jana katika kikao cha majumuisho alichokifanya mara baada ya kuhitimisha ziara yake ya siku nne mkoani humo ambayo aliianza tarehe 19/02/2018.
Amesema miradi mingi hususani miradi ya maji katika maeneo mengi mkoani humo haitekelezwi kwa wakati na katika kiwango cha ubora unaotakiwa kwa kuwa baadhi ya viongozi wamekuwa wakipeana miradi hiyo kwa kuzingatia undugu/ ukaribu wao badala ya kuangalia sifa zinazotakiwa.
“Miradi mingi ya maji imeshindwa kwenye baadhi ya maeneo kwa sababu mmepeana kindugu ndugu, mnashindwa kukemeana mnashindwa kusimamiana miradi haiendi, msiwadhulumu wananchi haki yao; mlizoea huko nyuma mnachukua fedha za miradi na hamfanyi lakini siyo sasa hivi” alisema.
Mhe.Makamu wa Rais aliwaagiza Wakuu wa Wilaya kuwasilisha taarifa yenye orodha ya miradi inayotekelezwa katika maeneo yao, mtu anayetekeleza, hatua iliyofikia, tarehe ya kumaliza mradi na ikiwa haijamalizika ioneshwe sababu za kutokamilisha miradi hiyo kwa wakati, lengo likiwa ni kutoa nafasi kwa vyombo vya dola kufanya kazi yake.
Aidha, amevitaka vyombo vya dola ikiwemo Taasisi ya Kuzui na Kupambana na Rushwa(TAKUKURU) kufuatilia Miradi mbalimbali ya maendeleo inayotekelezwa katika Halmashauri zote mkoani humo.
Sanjali na hilo Mhe.Makamu wa Rais amewataka viongozi mkoani Simiyu kufanya kazi kwa kushirikiana ili kuwaletea wananchi maendeleo katika maeneo yao.
Wakati huo Mhe.Makamu wa Rais amewapongea viongozi na wananchi Mkoani Simiyu kwa kufanya vizuri katika sekta ya Kilimo hususani Kilimo cha zao la pamba na akaahidi kuwa Serikali itahakikisha wakulima wanapata dawa za kuuwa wadudu waharibifu ili malengo ya kuongeza mavuno mwaka huu kufikia kilo milioni 300 yaweze kutimia.
Vile vile amewapongeza kwa kutekeleza Sera ya Tanzania ya Viwanda kwa kuanzisha viwanda katika maeneo mbalimbali kupitia Mkakati wa “Wilaya moja Bidhaa moja” ambapo amesema Serikali inakusudia kujenga Kiwanda cha Bidhaa za Afya zitokanazo na pamba (Bariadi) na Maji wanayotundikiwa wagonjwa(IV Fluid/Drip) katika wilaya ya Busega.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amehitimisha ziara yake jana Mkoani Simiyu ambapo alikuwa Mgeni Rasmi katika mahafali ya 34 ya Chuo kikuu Huria cha Tanzania yaliyofanyika Uwanja wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI KUHUSU HABARI HII FUNGUA HAPA:-https://simiyuregion.blogspot.com/2018/02/makamu-wa-rais-akemea-tabia-ya-kupeana.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa