Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amesema Simiyu itaendelea kufuata maelekezo ya Serikali katika mapambano dhidi ya maambukizi ya Virusi vya Corona, ikiwa ni pamoja na kuwatowaweka karantini wasafiri wanaotoka katika mikoa yenye maambukizi kama inavyopendekezwa na baadhi ya wananchi badala yake itawaweka wasafiri kutoka nje ya nchi.
Mtaka ameyasema hayo leo Aprili 17, 2020 wakati wa uhamasishaji wa zoezi endelevu la upuliziaji dawa kwenye magari ya abiria katika kituo kikuu cha mabasi Bariadi, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kupambana na maambukizi ya Virusi vya Corona, ambalo limeongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka.
“Tumeona kauli za viongozi mbalimbali, tumeona pia jumbe za watu wa Simiyu katika mitandao mbalimbali ya kijaamii ambao wangetamani watu kutoka katika mikoa yenye maambukizi wawekwe karantini sisi kama mkoa tunasema hapana, maelekezo yote kuhusu Corona yanatoka kwa Mhe. Waziri Mkuu na mpaka sasa wasafiri wanaowekwa karantini ni wanaotoka nje ya nchi,” alisema Mtaka.
Aidha, Mtaka ametoa wito kwa wananchi wa mkoa wa Simiyu kufika katika vituo vya kutolea huduma za afya na kutoa taarifa kwa wataalam wa afya pale wanapohisi kuwa na dalili zinazotajwa kwa mtu mwenye maambukizi ya Virusi vya Corona ili waweze kupata msaada stahiki wa kitaalam.
“Watu walioko karantini hawajasakwa na polisi tunao watu wanaotoka safari za mbali na kuja kuomba wenyewe watengwe, wengine familia zao zinaleta taarifa kuwa zina mgeni wa aina fulani na kuomba ajitenge, jamii zetu zimekuwa na uelewa wa kutosha kwani zinapoona mgeni zinatoa taarifa kwenye mamlaka husika nayo inachukua hatua,”alisema Mtaka.
Katika hatua nyingine Mtaka amesisitiza kuwa zoezi endelevu la upuliziaji dawa kwenye magari ya abiria lifanyike mapema bila kuathiri ratiba za wasafiri huku akiwataka makondakta kuhakikisha wanawasimia abiria wamenawa mikono yao kwa kutumia kwa kutumia maji yenye dawa . maji tiririka na sabuni na ambao wana vitakasa mikono wavitumie.
Mtaka amebainisha kuwa mpaka sasa Mkoa hauna mgonjwa mwenye maambukizi ya virusi vya Corona na kuongeza kuwa ni vema wananchi watumie siku tatu kuanzia leo Aprili 17, 2020 hadi 19 Aprili, 2020 zilizotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kumuomba Mwenyezi Mungu ili aweze kutuepusha na janga hili.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Dkt.Festo Dugange amesema hadi sasa jumla ya watu 120 kutoka nje ya nchi wamewekwa kwenye maeneo ya uangalizi maalum (karantini) katika mabweni ya shule za sekondari, ambapo watu 18 kati yao wameruhusiwa baada ya kumaliza siku 14 na kugundulika kuwa hawana maambukizi ya virusi vya ugonjwa wa homa ya mapafu (Corona COVID-19).
Kwa upande wake Kamanda wa Mkoa wa Simiyu, Henry Mwaibambe amewataka wananchi wa Mkoa huo kufuata maelekezo yaliyotolewa na serikali huku akiongeza kuwa jeshi hilo halitosita kuchukua hatua za kisheria kwa mtu yeyote ambaye atakiuka au kushindwa kufuata maelekezo.
Nelson Rambo ni kondakta wa basi la Kwangus Express linalofanya safari zake Bariadi -Mwanza amesema kuwa wanafuata maelekezo yaliyotolewa na serikali kwa abiria wanaopandia njiani kunawa mikono pamoja na kupuliza madawa kwenye mabasi.
Akizungumza kwa niaba ya abiria Rehema Mapalala ameishukuru serikali kwa zoezi hilo la upuliziaji wa madawa kwenye mabasi na kusema kuwa wamelipokea kwa furaha kwani linajali afya za wasafiri huku akiomba elimu iendelee kutolewa kwani siyo wananchi wote waliopata elimu ya namna ya kujikinga na virusi vya Corona.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI FUNGUA KIUNGANISHI HIKI:-https://simiyuregion.blogspot.com/2020/04/hatutaweka-karantini-wasafiri-wa-ndani.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa