Baraza la Uongozi wa Chuo cha Mipango Dodoma limeushukuru , uongozi wa Mkoa wa Simiyu kwa kukubali kutoa eneo la ekari 50 bure kwa ajili ya ujenzi wa Tawi jipya la chuo hicho , katika Kata ya Nyakabindi Halmashauri ya Mji wa Bariadi.
Shukrani hizo zimetolewa na Kaimu Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Mipango Bibi.Mugabe Mtani , katika mazungumzo maalum na viongozi wa Mkoa wa Simiyu muda mfupi kabla ya kikao cha Baraza hilo kilichofanyika mkoani Simiyu.
Kaimu Mwenyekiti wa Baraza la Uongozi wa Chuo cha Mipango Bibi. Mugabe Mtani ameshukuru kwa niaba ya Chuo hicho kwa kupewa eneo hilo ambalo litawawezesha kujenga miundombinu ya kutosha ya chuo hicho katika Mkoa wa Simiyu.
“Tunashukuru sana uongozi wa Mkoa wa Simiyu kwa kutupa hili eneo kubwa katika wakati huu ambao sisi tunaona ni wakati muafaka kwa sababu tulikuwa kwenye mkakati wa kutafuta eneo la kujenga, pale Mwanza tuna eneo ambalo kama tungelitumia lingetugharimu fedha nyingi kuliko hili la Simiyu kwa sababu liko kwenye mawe” alisema Mtani.
Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Chuo cha Mipango, Hozen Mayaya amesema iwapo chuo hicho kitakamilika kujengwa kitasaidia kutoa mafunzo ya maendeleo vijijini na hivyo kusaidia upatikanaji wa watalaam hapa nchini wakiwemo wa mipango pamoja na kusaidia katika ufanyaji wa tafiti mbalimbali.
Ameongeza kuwa upatikanaji wa eneo hilo utasaidia lengo la Chuo la kuwa vituo vingi kadri mahitaji yanavyoongezeka jambo ambalo litasaidia pia kusogeza huduma karibu na wananchi.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Bariadi ambako eneo hilo lipo, Bw. Melkizedeck Humbe amesema Chuo cha Mipango kitapojengwa Mkoani Simiyu kitakuwa msaada mkubwa kwa Mkoa huo ambao unajipambanua kwa Uchumi wa viwanda.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Mhe. Anthony Mtaka amesema kuwepo kwa chuo hicho kutaongeza hamasa ya elimu kwa vijana wanaomaliza elimu ya sekondari na kidato cha sita kujiunga na vyuo vya elimu ya juu ,huku akitoa wito kwa Taasisi zingine za umma na binafsi kuwekeza katika sekta ya elimu.
“ Sisi kama Mkoa tunatoa fursa kwa Wakuu wote wa Vyuo Vikuu hapa nchini wanaotaka kujenga matawi ya Vyuo vyao ili waondokane na kulipa fedha nyingi kwa ajili ya pango la majengo, mkoa wa Simiyu unawaakaribisha na tunawahakikishia upatikanaji wa Ardhi Bure” alisema Mtaka.
MWISHO:
KUPATA PICHA ZAIDI JUU YA HABARI HII FUNGUA HAPA:-https://simiyuregion.blogspot.com/2018/05/chuo-cha-mipango-washukuru-uongozi-mkoa.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa