Shirika lisilo la Kiserikali la AGPAHI limetoa msaada wa jumla ya vifaa 50 vya kupima joto mwili vyenye thamani ya shilingi 12,500,000/= kwa mkoa wa Simiyu kwa ajili ya kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi ya Virusi vya Corona.
Awali akizungumza kabla ya kukabidhi vifaa hivyo Mratibu wa AGPAHI Mkoa wa Simiyu, Dkt. Julius Sipemba amesema Shirika hilo limefuata maelekezo ya Serikali katika utoaji wa misaada ambapo amebainisha kuwa vifaa hivyo vimepitia wizara ya afya na kupata kibali cha kuvigawa katika mikoa ili vipelekwe katika vituo vya kutolea huduma.
Akipokea msaada huo kwa niaba ya serikali Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bw. Jumanne Sagini ameishukuru AGPAHI kwa kutoa vifaa vya kupima joto mwili na kusema kuwa awali Mkoa huo ulikuwa na uhaba wa vifaa hivyo; huku akibainisha kuwa vifaa hivyo vitasaidia hususani kwenye maeneo ambayo yalikuwa hayana ili kuwapima watu joto mwili kabla ya kuingia kwenye maeneo hayo.
Wakati huo huo Sagini ameushukuru Wakala wa Usambazaji Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Mkoa wa Simiyu kwa msaada wa vifaa vya kunawia mikono kuunga mkono juhudi za serikali, katika kuchukua tahadhari ya maambukizi ya Virusi vya Corona na kusisitiza kuwa vifaa hivyo vitapelekwa katika maeneo yenye mkusanyiko wa watu wengi.
“RUWASA ni taasisi mpya lakini pamoja na upya wake wamejinyima na kutoa shilingi 1,750,000/= kununua vifaa hivi ili kuokoa maisha ya watu; pamoja na kuhakikisha tunapata maji safi na salama wameona waunge mkono juhudi za serikali kuhakikisha watu wananawa na sabuni na maji tiririka kujikinga na Corona, mkoa tunatambua mchango wenu,” alisema Sagini.
Akizungumza kwa niaba ya Meneja wa RUWASA Mkoa wa Simiyu, Mhandisi Mahobe Mahuyemba amesema RUWASA kama wakala mpya umetoa msaada huo ikiwa ni sehemu ya kuonesha uhusiano wake na jamii katika kile kinachofanyika katika utekelezaji wa miradi m ya maji na uhalisia wa maisha ya watu huku akisisitiza kuwa vifaa hivyo kupelekwa katika maeneo yenye mikusanyiko ya watu ikiwemo shule na hospitali.
Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Dkt. Festo Dugange amewashukuru AGPAHI na RUWASA kwa msaada huo kwa jamii ya watu wa Simiyu huku akibainisha namna mkoa wa Simiyu ulivyonufaika na uwepo wa AGPAHI kama wadau muhimu wa afya.
“Kama mkoa tumekuwa tukishirikiana na AGPAHI kuboresha huduma za afya katika nyanja mbalimbali ikiwemo kuboresha huduma za afya kwa watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI kwa kutoa huduma za matibabu, kujenga uwezo kwa watoa huduma wanaowahudumia, kutoa magari kwa ajili ya usimamizi shirikishi na kujenga miundombinu yakiwemo majengo,” amesema Dkt. Dugange.
MWISHO
KUPATA PICHA ZAIDI FUNGUA KIUNGANISHI HIKI:-https://simiyuregion.blogspot.com/2020/06/agpahi-ruwasa-watoa-msaada-wa-vifaa-kwa.html
Bariadi - Somanda
Anuani ya Posta: S. L. P. 4, BARIADI.
Simu ya Mezani: 028-2700011/2700054
Simu ya Mkononi: 028-2700011/2700054
Barua Pepe: ras@simiyu.go.tz
Hati Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Simiyu.Haki Zote Zimehifadhiwa